Ads Top

UKAMILIFU WA NENO LA MUNGU


UKAMILIFU WA NENO LA MUNGU


Mithali 30:5-6
Kila Neno la Mungu limehakikishwa; Yeye ni ngao yao wamwaminio.
Usiongeze neno katika maneno yake; Asije akakulaumu, ukaonekana u mwongo

Neno la Mungu ni kamilifu. Halina mapungufu. Halichuji. Halijapungua. Limekamilika na limethibitika vizazi na vizazi. Neno llote linalotoka katika kinywa cha Mungu liko sahihi na limekamilika. Limekamilika kwani Mungu mwenyewe ni mkamilifu. Ni sahihi kwani Mungu mwenyewe ni Kweli na hana hila ndani yake. Nimekuwa natafakari jioni n usiku huu kuhusu UKAMILIFU WA NENO LA MUNGU na hasa baada ya kusoma Mithali 30:5-6 na nikashituka sana. Mara ya kwanza nilidhani nimeelewa. Lakini nikagundua sijaelewa. Ni maneno ambayo siyo mara ya kwanza kuyasoma ila nimeyasoma tena leo na nimeona kitu cha kutafakari na kujifunza. Nikapata maswali kadhaa:

1. Nani aliyelihakikisha kila neno la Mungu?
2. Nini maana ya kuongeza au kupunguza kutoka kwenye alichosema Mungu?
3. Nitajuaje nimepunguza au nimeongeza?

Wakati natafakari hii, nikaenda Ufunuo 22:18-19, nikashangaa Zaidi kwamba sura ya mwisho kabisa ya kitabu cha mwisho kabisa kilichobeba mwisho wa kila mwanzo kina maneno hayo hayo tena kwa mkazo mkubwa Zaidi. Ila nimeogopa. Maana nawaza hivi Mungu akinilaumu ndo inakuwaje sasa, yaani naonekana muongo kwa sababu nimepunguza au nimeongeza maneno yangu juu au chini ya neno la Mungu kwasababu zangu mwenyewe. Ujinga ni kitu kibaya sana. Ubinafsi na ujinga ni mapacha. Nikaenda kusoma Ufunuo.

Ufunuo 22:18-19
Namshuhudia kila mtu asikiaye maneno ya unabii wa kitabu hiki, mtu yeyote akiyaongeza, Mungu atamwongezea hayo mapigo yaiyoandikwa katika kitabu hiki. Na mtu yeyote akiondoa lolote katika maneno ya unabii wa kitabu hiki, Mungu atamwondolea sehemu yake katika ule mti wa uzima, na katika ule mji mtakatifu, ambao habari zake zimeandikwa katika kitabu hiki.

Nimeshituka sana. Kupunguza au kuongeza juu ya kile amesema Mungu kinaweza kunigharimu kukosa lile tumaini letu la milele? Nimewaza, kama tu mapigo yaliyomo kwenye kitabu cha ufunuo yanaogopesha hata kusoma tu, sasa ndo niongezewe kiuhalisia kisa nimeongezea juu ya alichosema Mung undo nitakuwaje sasa. Nimejihurumia sana. Kama kuondoa au kupunguza toka kwenye yale ambayo biblia imeweka kunaweza kunifanya si tu sehemu yangu kuondolewa kwenye mti wa uzima bali pia niwe sina sehemu katika ule mji mtakatifu, sasa ndo inakuwaje. Nashindwa kujua hali yangu niko wapi kwani bado hata sijui kuongeza au kupunguza ni kufanyaje. Hapo kwenye mapigo ikabidi nikasome japo msitari mmoja tu kwenye Ufunuo 15:1, nikakutana na mapigo saba ambayo ndio ukamilifu wa mapigo ya Mungu. Nikiwa naendelea kuwaza na kulitafuna hili, nikaiona Kumbukumbu 4:2. Nikaisoma:

Kumbukumbu 4:2
Msiliongeze neno niwaamurulo wala msilipunguze, mpate kuzishika amri za Bwana, Mungu wenu, niwaamuruzo.

Huu msisitizo ninaoupata hapa unanifanya nijione MJINGA FIRST CLASS PREMIUM. Ni mambo mawili tu nayaona hapo, kupunguza au kuongeza. Nikiona naumia napunguza au kuongeza ili njisikie nafuu na ili nisione kama nahukumiwa badala ya kurekebishwa. Hii tafakari ikanisukuma mbele kwenye Kumbukumbu 12:32 ambapo anasema neno hili niwaagizalo lolote liangalieni kulifanya; usiliongeze, wala usilipunguze. Mungu wangu. Najiuliza tu kwanini Mungu hataki neno lake lipunguzwe au liongezwe. Mungu ni MKAMILIFU,HAITAJI NYONGEZA WALA PUNGUZO. Ni kama najaribu kujiridhisha kuwa Mungu angekuja dukani kwangu kununua kitu asingeomba apunguziwe bei kwani anao utoshelevu wa utajiri. Najifunza kwa maumivu ila ndo nashindwa kkuacha kujifunza ila inauma sana kwani kuna wakati natamani nilifanyie marekebisho neno ili liendane na kile ninataka. Kama nataka sadaka basi ujanja ujanja mwingi sana. UBINAFSI NA UJINGA NI MBEGU ZA UHARIBIFU. Nikakumbuka Yoshua 1:7. Nikasoma:

Yoshua 1:7
Uwe hodari tu na ushujaa mwingi, uangalie kutenda sawa sawa na sharia yote aliyokuamuru Musa mtumishi wangu; usiiache, kwenda mkono wa kuume, au wa kushoto, upate kufanikiwa sana kila uendako.

Nikawa najiona vile ilivo rahisi kutolewa kwenye nafasi ya kufaidi Baraka za Mungu na kumfaidi Mungu mwenyewe kwasababu tu sitaki kuonekana sijui. Nataka nionekane nina maufunuo ya ukweli na vile naishi kwenye kizazi cha mitume na manabii. Hapo nikaona kumbe kufanikiwa kwa Yoshua hakukuwa na uhusiano wa kuwa maarufu na vipaji vya kujifunza na kupewa tuzo. Maelekezo na maonyo yako yamenyooka hapo najisomea. Yoshua alipewa kufanikiwa kila aendako lakini kama tu akifanya kama alivyoambiwa, asiende kulia wala kushoto, yaani asitoke nje ya neno la Mungu, asipunguze wala kuongeza kitu bali aelekeze macho yake kwenye neno. Nikiwa naliwaza hili, nikaiona Mathayo 23:13. Nikaanza kuisoma, japo kwa mbali najisikia kama kisu kinapita kwenye moyo.

Mathayo 23:13
Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwakuwa mnawafungia watu ufalme wa mbinguni;  ninyi wenyewe hamuingii, wala wanaoingia hamuachi waingie.

Ukisoma huo msitari unaweza kusema kuna watu maalum, yaani makonkodi wanazungumziwa, yaani mafarisayo na waandishi. Ni kweli. Ila nikawa najiwazia mwenyewe, mimi ni mwandishi na farisayo kwa kiwango gani? Kujua kiwango nikajiuliza ni mambo gani au tabia gani au atendo gani nayafanya au kuwaambia na kuwafundisha wengine ambayo kimsingi yanawazuia kuingia kwenye ufalme wa Mungu? Ila lililoniogopesha ni hiyo kwamba mtu akijua haendi mjini ni rahisi sana kuficha pasi ili anaeenda na hajaanyoosha nguo iwe vigumu na yeye kwenda. Nimewaza sana, je hii Mathayo 23, hapo inaposema MNAWAFUNGIA watu ufalme wa mbinguni inaweza pia ikawa inamaanisha mafundisho potofu yanayowafanya watu wakosee njia na wapiti NJIA PANA badala ya NYEMBAMBA ambayo wachache huiona? Ndo hapo Mathayo 7:13 na 14 ikalia moyoni. Nikaona ngoja nimalizie na Mathayo 23:15. Nikaanza kusoma:

Mathayo 23:15
Ole wenu waaandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwakuwa mnazunguka katika bahari nan chi kavu ili kumfanya mtu mmoja kuwa mwongofu; na akisha kufanyika, mnamfanya kuwa mwana wa jehanam mara mbili Zaidi kuliko ninyi wenyewe.

Mungu wangu wee. Naomba rehema na msahamaha mimi Raphael. Inawezekanaje kuwahubiria watu na kuwafanya wongofu halafu wakishafanyika wafanyike tena kuwa wana wa Jehanam mara mbili Zaidi kuliko aliyewafanya? Nikawaza sio kwa kupunguza na au kuongeza juu ya neno la Mungu kweli? Na huu udanganyifu wa mali na utajiri ulioingia kanisani leo hii? Ndio nikawaza, yanipasa kuwa makini sana ninapoamua kuwa chini ya mtu fulani hata kama ni maarufu kuliko dhambi. Ndipo nikawa najichunguza, hivi walio chini yangu wanajua hili? Nikajifunza na kuona ngoja na wao wajifune pamoja na mimi tukiendelea kutafuta majibu yay ale maswali yangu matatu niliyoanza nayo pale mwanzoni. Siku nikipata jibu ya hayo maswali badi nitaandika tena. Na wewe mwenzangu na mimi ukipata jibu basi andika ili tujifunze wote.

NAJISALIMISHA KWAKO YESU, MIMI RAPHAEL JL:

By Raphael JL:
078711003(Whatsapp)
www.fichuka.blogspot.com

Hakuna maoni:

Inaendeshwa na Blogger.