Ads Top

MKUU WA WANYWESHAJI HAKUMKUMBUKA YUSUFU



Alimsahau. Alimsahau. Alimsahau. Hakumkumbuka. Pamoja na Yusufu kumuomba, alimuomba akawambia “ila unikumbuke mimi, utakapopata mema, ukanifanyie fadhili, nakuomba, ukanitaje kwa Farao, na kunitoa katika nyumba hii” Mwanzo 40:14. Pamoja na maneno hayo mazito ya kumuomba yule Mkuu wa Wanyweshaji wa Farao lakini bado jamaa alimsahau na kwakweli hakumkumbuka. Inauma sana. Inaboa na kukera sana. Inakatisha tama asana. Inaumiza nafsi sana na inaweza kukukatisha tamaa ya kutokuendelea kuwasaidia watu. Huyu Mkuu wa Wanyweshaji, aliota ndoto na hakujua tafsiri yake. Yusufu alimtafsiria ile ndoto kuwa baada ya siku tatu atatolewa na kurejeshwa kwenye nafasi yake kama hapo kwanza. Na kweli, baada ya siku tatu jamaa akatolewa gerezani na kurudishwa kwenye nafasi yake ya mwanzo. Mwanzo 39, 40 na 41.

Wewe fikiria jamaa karudi kwenye nafasi ambayo alikuwa ndo anaesimamia mambo ya vinywaji vyote anvyokunywa Yusufu. Yeye ndo Mkuu wa hicho kitengo, kama alivyokuwepo yule jamaa mwingine ambaye alikuwa Mkuu wa kitengo cha kutengeneza Mikate. Leo amerudi kwenye nfasi yake, karibu kabisa na Mfalme. Huyu ni mtu mwenye ushawishi mkubwa sana kwa Mfalme na ndio maana Yusufu alimuomba na kumsihi sana kwamba asimsahau akisharudi kwenye kiti chake. Matarajio ni hayo tu kwamba jamaa angemkumbuka Yusufu ili nae atolewe gerezani kwani alienda huko kwa kusingiziwa. Ni kweli kwamba alisingiziwa lakini bado alienda gerezani ingawaje alivyokuwa huko alipata kibali toka kwa mkuu wa gereza. Lakini bado, kikubwa cha kuweka akilini ni kwamba Yusufu alienda gerezani kwa kusingiziwa na Mungu aliona hayo yote.

Ngoja nikutafakarishe jambo. Yusufu alisahauliwa na mwanadamu aliemsaidia kutafsiri ndoto yake gerezani lakini hakusahauliwa na Mungu aliye mpa kibali n ahata uwezo wa kutafsiri ndoto kule gerezani. Kibinadamu lazima ilimuuma Yusufu, kuona miaka miwili imepita na bado hatoki tu na hapo ilikuwa wazi kabisa kuwa jamaa alishamsahau. Kuthibitisha kuwa Mungu hakumsahau Yusufu, kama miaka miwili hivi baadae, fursa nyingine ya kutafsiri ndoto ya Farao inakuja na watu wote ambao Yusufu alitegemea wangeweza kumtafsiria ile ndoto walishindwa. Ndiposa, yule yule ambaye Yusufu alitaka amsaidie pale mwanzo  ambapo alitarajia kusaidiwa, anaibuka tena hapa na tunaona anasema hivi “nayakumbuka makossa yangu leo” Mwanzo 41:9.

Kwenye majira na nyakati zilizo amriwa, kwenye mazingira sahihi na sababu sahihi na watu sahihi tunaona yule yule Mkuu wa Wanyweshaji akitimiza ahadi yake japo kwamba alisahau kwa muda mrefu. Ni lazima iwe kwenye majira sahihi. Iwepo sababu sahihi. Awepo mtu sahihi. Kwenye majira hayo tunaona imeandikwa hivi “Ndipo Farao akapeleka watu, akamwita Yusufu, wakamleta upesi kutoka gerezani. Akanyoa, akabadili nguo zake, na kuingia kwa Farao” Mwanzo 41:14. Ni hayo tu. Kibali ambacho Yusufu alikisubiria kwa miaka miwili hatimae kimekuja kwa wakati wake. Fursa. Kwa Yusufu alikuwa na uwezo aliopewa na Mungu wa kutoa maana za ndoto. Hii ilikuwa fursa ama mtaji. Ngoja tutweke mpaka kilindini hapa tuone.

Kwa kuangakia hityo story niseme machache hapa. Huenda wewe ni Yusufu. Unasingiziwa sana na kuonewa sana ila BWANA YUKO PAMOJA NA WEWE. Hicho ndo kikubwa ambacho kilimtofautisha Yusufu na wenginewe wote. Huenda kuna watu umewasaidia kwa njia moja au nyingine. Walikutegemea kipindi fulani cha uhitaji wao. Walihitaji uwape maana ya ndoto au uwaambie maana ya mambo yanayotokea kwenye maisha yao. Na wewe ulifanya yote kwa Bwana amekupa uwezo huo. Huenda mtu ulisoma nae na mlikuwa marafiki sana tu. Mkawekeana ahadi za kusaidiana kufa kupona katika maisha. Huenda wakati huo mnawekeana ahadi za urafiki wewe ndo ulikuwa msaada wake. Huenda. Kama hauko upande wa kwanza wa huenda basi uko upande wa pili yake. Ngoja tuone. Lakini.

Yule uliemsaidia huko nyuma, uliedhani angemwambia Mfalme habari zako ili na wewe uitwe, sasa ameinuliwa na yuko mahali pa juu. Sasa amekuwa mkuu wa kitengo fulani. Sasa amekuwa karibu na wakuu wanaofanya maamuzi fulani. Sasa amekuwa mtu mwenye watu chini yake na anaweza kuamuru lolote na likawa. Ni kweli mlikuwa wote kwenye kazi moja na mlipatana sana. Yeye akapata kibali akaenda mbele yako. Yuko kwenye nafasi za kifalme. Anakula pamoja na wakuu. Anawasiliana nao kama alivyokuwa anawasiliana na wewe pale zamani ila sasa unapiga mara mia na simu haipokelewi wala kujibiwa. Kinauma sana, haha haha hahaha. Swali ni moja tu, JE BWANA YUKO PAMOJA NA WEWE?

Naomba uelewe kwamba, huenda majira yako ya wewe kupelekwa kule unakotaka bado hayajafika. Usimchukie huyo mtu kwani na yeye hafanyi tu kwa sababu wewe ulimsaidia bali juu ya yote yapo MAJIRA YA MUNGU. Pia usisahau kuwa lipo KUSUDI LA MUNGU kwako na kwake. Kuna vitu ukipewa kablha hujajiandaa unaweza kufa au kuharibika na watu wakabaki wanashangaa. Usimlaumu. Yusufu alisubiria miaka miwili mbele, ila aliye mtaja kwa Farao ni yule yule ambaye alimsahau kwa miaka miwili. Subiri. Majira yako yanakuja. Ipo fursa mbele yako. Kisikuume mpaka ukakosana na mtu kana kwamba yeye ni Mungu Msaidizi.


Ulidhani angekuunganishia na wewe upate kazi au upate hata kazi ya muda lakini unaona jamaa anawasaidia wengine kuliko wewe. Wewe bado muda haujafika. Usiiache Imani. Usiache kumwamini Mungu. Kumbuka, AMTEGEMEAE MWANADAMU AMELANIWA ila ujue kuwa Mungu anawatumia wanadamu wazuri na wabaya kutupa urithi wetu. Sasa wewe tulia. Ulidhani umesubiri kupata kazi mpaka umechoka? Umesubiri kupata uzao wa tumbo lako mpaka umechoka? NOTHING HAPPENS BY CHANCE. Hakuna linalotokea kwa kubahatisha kwako. Wewe huishi kwa bahati nasibu. Maisha yako yalipangwa. Yaliandaliwa. Yalitengenezwa. Fikiria Mungu anavyokutazama wakati unahangaika na hivyo vitu.

Basi itoshe kuwakwambia kuwa RUSA YAKO INAKUJA. Achana na WANYWESHAJI, fahamu kuwa majira yakifika na wewe utatajwa mbele za mfalme. Utapata ulichokuwa unahitaji. Mwamini Mungu. WANYWESHAJI BANA, haha haha haha haha.

Na Raphael Joachim Lyela (Raphael JL:)
0767033300
faryesu@hotmail.com
www.fichuka.blogspot.com
instagram@raphaellyela
facebook@Raphael Joachim Lyela
Dodoma. Tanzania. Afrika Mashariki.

Hakuna maoni:

Inaendeshwa na Blogger.