Ads Top

MACHO YA MOYO NI UFAHAMU WAKO.



18.01.2018

Zaburi 119:18 “Unifumbue macho yangu niyatazame maajabu yatokayo katika sheria yako.
Ni maombi yenye nguvu na yanayofunua shauku ya kweli ya Mzaburi. Alionyesha ana kiu  na njaa ya neno la Mungu. Alionyesha kuwa, kwake neno linalotoka kwenye kinywa cha Mungu ndio kila kitu. Anajua ndani ya sheria za Mungu kuna nini. Mzaburi anaomba kufumbuliwa macho ili awe na uwezo wa kutazama maajabu yaliyomo ndani ya sheria ya Mungu. Ameomba kufumbuliwa macho, sio kupewa maono mapya. Ni kama alijua kuwa tatizo sio kuona mambo mapya au kama mtu anataka kuona mambo mapya ni lazima macho yake yafumbuliwe.

Hii inamaanisha kuwa, alijua kuna shida kwenye macho yake na pia alijua Mungu anaweza kumsaidia hiyo shida yake. Macho yake yalikuwa hayawezi kuona. Kumbuka kuwa aliomba kufumbuliwa macho hakuomba kupewa mcho mengine mapya. Aliomba yle yale macho alokuwa nayo yafumbuliwe ili kazi ya macho idhihirike. Yaani kama una macho lakini huoni sasa macho yana kazi gani maana kazi ya macho ni kuona? Haya macho lazima yawe macho ya tofauti sana. Kwa upande wa pili ipo sheria ya Mungu au neno lake ambapo ndani yake kuna MAAJABU au mambo ya kushangaza, mambo makubwa nay a kustajabisha.

Mzaburi alijua mambo yaliyoko ndani ya neno la Mungu kwa kiwango ambacho ilikuwa shauku yake kuomba afumbuliwe ili ayaone hayo maajabu yenyewe. Lazima atakuwa alikuwa ameshaona kwa sehemu maajabu haya na ndo maana akawa na shauku sana ya kuomba namba hii. Hakika aligundua siri nzito na nzuri san ahata kwetu leo. Hapo unaona mambo makubwa mawili. Moja unaona swala la macho yake kuwa na shida lakini la pili unaona kuwa kumbe ndani ya neno la Mungu kuna mengi tusiyoyajua na ambayo kuyajua kwake ni lazima macho yashughulikiwe kwanza.

Macho. Ukisoma Waefeso 1:18 utaona kuwa moyo una macho, na haya macho ya moyo yanatakiwa yatiwe nuru ili tupate KUJUA. Shika hilo neno kujua, kwani kwenye Zaburi inasema macho yakifumbuliwa basi mtu ATATAZAMA maajabu. Kumbe haya sio mcho ya kawaida. Haya ni macho ya ndani, wengine husema ufahamu. Macho lazima yatiwe nuru, yaani yafumbuliwe. Kumbe kinachofumbua macho yetu ni nuru au neno la Mungu mwenyewe na baada ya hapo ndipo tunaanza kuelewa namna Mungu anavyofanya kazi.

Maajabu. Ndani ya neno la Mungu utapata maajabu ya neno lake, hekima yake, ufahamu wake, uponyaji wake na ushauri wake kila siku. Zipo siri zilizofichwa ndani ya neno lake. Na kuzijua siri hizi ni lazima mtu uwe na kiu na njaa na shauku. Hujiulizi kwanini kusoma na kutafaari neno la Mungu kuna vita? Kusinzia au kuchoka ukianza tu kusoma neno. Hii ndio sababu kwanini viwango vimelegezwa sana. Ila Mungu ni mwaminifu na anaweza kutusaidia na kutuvusha tukimuomba.

For the King and His Kingdom,
Pastor Raphael JL:
0787110003.
DODOMA.

Maoni 1 :

  1. Aisee Sijapata kuelewa hapo mwanzo, kuhusu hili neno, kuna vitu nimeongeza kwenye ufahamu sikupata kuvijua hapo mwanzo.

    Ubarikiwe Sana mwalimu Raphael

    JibuFuta

Inaendeshwa na Blogger.