Ads Top

SHUHUDA ZA MUNGU NDANI YA MAISHA YAKO YA KILA SIKU.



15.02.2018
Zaburi 119:46
 Nitazinena shuhuda zako mbele ya wafalme, wala sitaona aibu.
Tafakari ya msitari huu inafanana kabisa na Mathayo 10:18 na Matendo 26:1,2. Kwenye Mathato 10, inasema nanyi mtachukuliwa mbele ya maliwali na wafalme kwa ajili yangu, kuwa ushuhuda kwao na kwa mataifa. Wazo hilo hilo tunaliona pia kwenye Matendo 26, Paul alisimama mbele ya mfalme Agripa na kujitetea mbele yake baada ya kushitakiwa kuhusu habari njema aliyokuwa anaisema na juu ya Imani yake. Zaburi hii inatukumbuka jambo muhimu sana, kutokuona aibu kwa ajili ya matendo makuu ya Mungu katika maisha yetu ya kila siku popote tutakapokuwa ikiwemo wakuu au wafalme.

Hili kundi la wafalme ni kundi la wafanya maamuzi na wasimamizi wa sera na sheria pia na kwa namna fulani kusimama mbele ya watu hawa na kuanza kusema kuhusu Mungu inahitaji uwe umejitoa sana. Wewe fikiria unataka kuzishuhudia shuhuda za Bwana kwa rais au mbungu au waziri, itakuwa rahisi kwa kiwango gani? Kinacholeta ugumu ni hiyo mamlaka waliyonayo hawa watu na kwa hiyo kuwafikia bila aibu ni lazima hakika usiwe upande wa aibu yenyewe.

Lazima kuwe na sababu ya kufanya mtu ashindwe kuzishuhudia shuhuda za Bwana mbele ya wafalme. Labda unaogopa kuonekana na wewe ni mpendwa au unaogopa kuonekana mshamba au unaogopa kupigwa au vyovyote vile itakavyokuwa. Kwa upande huu kama kweli mtu anazijua shuhuda za Mungu basi ni wazi kuwa atazisema na kama hazisemi na anazijua hiyo inamaanisha kuwa huenda yuko ule upande wa aibu au sababu za namna hiyo. Tunashindwa kutambua kuwa kusimulia wema ambao Mungu ameufanya kwenye maisha yetu kuna faida kubwa sana kwetu na kwa wale wanaotuzunguka.

Mpaka hapa tulipofikia katika maisha yapo mengi mema, mazuri na makubwa ambayo Mungu ametutendea sisi wanadamu tukianza na uzima tulionao lakini sisi huwa tunasahau hayo na tunaona ni kwa akili zetu au wakat mwingin tunaona aibu kuyasema mbele za watu kwa hofu ya kuonekana mshamba. Ukweli uliopo hapo ni kuwa hizo zote  shuhuda za Bwana, yaani jumla ya mambo yote yanayotafsiri Mungu alivyo, anavyofanya kazi pamoja na sifa zake zote. Pia ni muhimu  kujua kuwa ipo nguvu ndani ya ushuhuda wa shuhuda za Mungu inayoweza kutenda makuu sana kwa anaesikia, kumbuka pia kuwa Imani chanzo chake ni kusikia neno la Kristo.

Ukipata fursa ya kuzinena shuhuda za Bwana mbele ya wakuu basi fanya hivyo kwani wewe unaweza kudhani watu hao wana utoshelevu lakini kumbe sio utoshelevu wa kila kitu. Ni kweli wanayo mamlaka ila hawana amani, wangehitaji kusikia jinsi Mungu unaemwabudu wewe huwapata wanadamu amani ipitayo fahamu na akili za wanadamu. Leo tena, tumuombe Mungu atusaidie sana. Atuumbie ujasiri na kutupa ufahamu kwa neno lake ili tuweze kufanya yale tunayopaswa kuyafanya.


For the King and His Kingdom,
Pastor Raphael JL:
0787110003.
DODOMA.

Hakuna maoni:

Inaendeshwa na Blogger.