Ads Top

*UNAPOTAFUTA MAFANIKIO, KUMILIKI NA KUTAWALA HAPA DUNIANI ZINGATIA .....



*_Mathew 4:9_*
*_And saith unto him, All these things will I give  thee, if thou wilt fall down and worship me._*

Shetani alimjaribu Bwana Yesu katika maeneo matatu makubwa:

1. Chakula au TAMAA ZA MWILI, *Matahyo 4:3*, ambapo Yesu alimshinda Shetani kwa kutumia NENO LA MUNGU kama unavyoona hapo msitari wa nne, *Kumbukumbu 8:3*. Hapa Shetani alimjaribu Yesu kwa chakula kwani Yesu alikuwa na njaa ya mfungo wa siku 40 kavukavu.

2. Mwenendo wa Maisha kwa ujumla au fahari ya maisha, KIBURI CHA UZIMA, *Mathayo 4:5-7*, ambapo pia Yesu alimshinda Shetani  kwa kutumia NENO LA MUNGU, *Kumbukumbu 6:16.* Hapa Shetani alitaka Yesu amjaribu Mungu kwa kujirusha chini. KAA MBALI NA KIBURI maana shetani anaweza kutumia uwezo wako kukuharibu na kukukosanisha na Mungu aliyekupa huo uwezo.

3. Fahari ya dunia, mali na milki zake, TAMAA YA MACHO, *Mathayo 4:8-10*, hapa Shetani aliahidi kumpa Yesu sehemu ya fahari ya dunia hii kwani alimpeleka katika kilele cha mlima na kumuonyesha fahari ya dunia. Hii fahari ni kila aina ya utajiri, mali, maana yake uchumi. Lakini pia mifumo ya kiutawala pamoja na siasa zake, dola pamoja na kumiliki milki za majengo kwa ujumla wake.

Katika kila jaribu, kasoro la mwisho Shetani alitumia maandiko hata kama ni kwa kupindisha. Cha ajabu Shetani alikuwa tayari kumpa Yesu fahari yote ya dunia, dunia ambayo Shetani ndio mungu wake, *Waefeso 2:2* lakini fahari ya dunia ilikuwa si kitu ukilinganisha na ushirika wa Bwana Yesu na Mungu. Kumiliki mali sio dhambi, tatizo ni njia ya kuzimiliki. Unapoendelea kutafuta mafanikio kwa kila njia, hakikisha unabaki katika njia ya mapenzi ya Mungu. Usikubali tamaa ya mwili, iwe ni chakula au mavazi nk; au kiburi cha uzima iwe ni majivuno na kiburi kwasababu ya uwezo, vipawa na karama na vipaji ulivyo navyo au ni tamaa ya macho iwe ni uchu wa madaraka ya kutawala, kumiliki mali n.k. vikuharibie uhusiano wako na Mungu.

Bahati mbaya au nzuri, dunia ya leo imejaa hayo maeneo matatu. Ni kweli Shetani anavyo hivo vitu, sharti lake kuu ni moja tu, UKIANGUKA NA KUMSUJUDIA, ANAKUPA VYOTE. Na ndio maana unaona dunia inavyowataabisha vijana wanaopenda umaarufu, wanaopenda kumiliki mali, magari na majumba ya kifahari; vijana hawa wako tayari kuua mashabiki wao, kuua wazazi na watoto wao ili mradi tu watoe kafara kwa shetani maana huko ndiko KUANGUKA NA KUMSUJUDIA NA KUMWABUDU. Karibia kila kijana anataka kuwa na Maisha ya kifahari, awe na gari kali, aweze kusafiri kwenda dunia nzima, awe maarufu akiwa na FOLLOWERS, SUBSCRIBERS wa kutosha kwenye mitandao ya kijamii maana anatafuta pesa. Kuwa na mambo haya sio shida, shida ni kwamba TAMAA YA MWILI, KIBURI CHA UZIMA NA TAMAA YA MACHO inawafanya vijana wengi kumwabudu Shetani na kweli tunawaona ni matajiri hata kuliko umri wao au kazi wanazofanya, ila ndani yao wanajua kinachoendelea.

Tuko kizazi kigumu sana kusikia na ndio maana unaona uasherati na uzinzi, sehemu ya TAMAA YA MWILI vimeshika kasi. Kila kukicha ni habari za ngono, picha za ngono, muziki umejaa matusi ya ngono lakini ndio nyimbo zinazopendwa zaidi. Natoa wito kwako wewe msanii, uwe wa nyimbo za injili au zisizo za injili, ITAKUSAIDIA NINI KUIPATA DUNIA YOTE NA KUIPOTEZA NAFSI YAKO? angalia kinachomtokea R Kelly sasa, kilichomtokea Michael Jackson au Kanye West, unadhani wewe una tofauti na wao?

BASI UNAPOTAFUTA MAFANIKIO *MATHAYO 6:33* ITAKUFAA. MAFANIKIO YA KISHETANI HAYANA MWISHO MZURI HATA KIDOGO.

Kwa ushauri,
Raphael Lyela-0744644699 (Whatsapp tu).
Instagram@raphaellyela
www.fichuka.blogspot.com

Hakuna maoni:

Inaendeshwa na Blogger.